Artists News in Tanzania

‘Kwa Heri Mwaka 2015 Karibu 2016’ Makala Inayochambua Tasnia ya Filamu 2015

Jacob-531

JB mmoja kati ya wasanii wa filamu

UMEMALIZA mwaka 2015 tupo mwaka 2016 ambao kuna baadhi wanajenga matumaini huku wengine wakisubiri kama mimi kuona majaliwa ya mola kama kutakuwa nan a unafuu au ndio balaa zaidi katika tasnia ya filamu mwaka jana hali haikuwa shwari baada ya wasanii kupotea.

Soko la filamu limeshuka sana huku kukiwa na sababu ambazo si za kitafiti zaidi ya shutuma kila upande ikiwa ni serikali au wadau wenyewe wa filamu, hali ni mbaya zaidi pale ambapo katika nchi yenye watu zaidi milioni arobaini kushindwa kuuza nakala laki tano tu.

Wasambazaji wa filamu wanasema kuwa wanauza nakala 10,000 tu na kwa filamu kubwa kama za akina JB, Nisha na Ray ndio wanaweza kudunduliza hadi nakala 20,000 na kuendelea kidogo, sijui lakini kwani kila nikipita mtaani na katika vibanda umiza naona sinema za Kibongo zikitamba.

Maswali ni mengi kuliko majibu labda ujio wa Serikali ya Tano wanaweza kupata dawa ya kutibu ugonjwa huu ambao unawashinda madaktari kila uchwao, nilisikia suala la mirabaha kwa wasanii.

Lakini kabla ya huko kwenye mirabaha kwanza iangaliwe njia sahihi ya ukukusanyaji kwani baadhi ya wasanii hawana imani na chombo chao cha haki miliki na Haki shiriki (COSOTA) kila kikucha kuna malalamiko kuhusu ulinzi wa haki zao.

Tuangalie zaidi katika filamu kwanini Filamu zimeshuka hata watu wengine kusingizia kifo cha marehemu Steven Kanumba ndio sababu kushuka kwa soko hilo ambalo liliweza kuondoa kabisa soko la filamu za Kinaijeria, tunahishi kwa hisia zaidi kuliko utafiti.

Wasanii
Wasanii kwa mwaka uliopita walijichanga katika masuala ya siasa na kuingia hata katika kugombea nafasi mbalimbali za uongozi lakini kwa bahati mbaya hakuna hata msanii mmoja ambaye aliibuka kidedea katika nafasi ambazo waliomba ridhaa kupitia vyama mbalimbali.

Mpambano wa CCM na Ukawa ulishika nafasi na kuwachanganya wasanii na kuingia katika bifu kati ya wao na wao huku wengine ambao ni waoga na waliwahi kuingia chama tawala kwa kufitinisha wenzao kwa kusema ni wapinzani na kuzua tafrani.

Wasanii hao ni Steven Mengele ‘Steve Nyerere’ aliyegombea Ubunge Jimbo la Kinondoni na kukosa, Irene Uwoya(Viti maalum) Tabora, Wastara Juma Morogoro (Viti Maalum),Wema Sepetu Singada (Viti Maalum) hawa waligombea kupitia CCM.

Wengine ni Mohamed Mwikongi ‘Frank’ aligombea Ubunge Segerea kupitia ACT Wazalendo, Rashid Mwinshehe ‘Kingwendu’ kupitia chama cha Wanachi CUF hawa walipigana katika majimbo yao lakini mambo hayakuwa mazuri kimsingi utaona wengi walikuwa chama CCM lakini hawakupenyeza.

Harakati hazikuishi hapo kwani hata baada ya kushindwa pia baadhi ya makundi yalishiriki katika kampeni ambazo kwa mwaka huu zilikuwa na ushindani mkubwa nap engine kujikuta wakiwagawa wapenzi wa kazi zao bila kujua.

Lakini wengine wanasema hawakuwa na jinsi iliwapasa kuingia huko katika kutengeneza maslahi mengine baada ya kukosa katika filamu kutokana na soko kuyumba na kwa upande huo walioingia CCM walifanikiwa kwani hali haikuwa shwari .

Mwaka mpya huu wamejipangeje? Hili ni swali muhimu sana kwa bahati mbaya hakuna wakujibu kwani sote tunaishi kwa mazoea mara nyingi watayarishaji wakishamaliza kutengeneza wanajikuta suala la promotion na masoko hawajihusishi navyo.

Tico muongozaji na mtayarishaji wa Filamu

Wasambazaji
Kwa upande wa wasambazaji ndio waathirika wakubwa kukwama kwa soko la filamu, ukiongea nao wanasema moja ya kikwazo kikubwa kwao, kati ya maduka yanayouza filamu kama yapo sabini basi yanayouza filamu za Kibongo ni matatu huku hayo yanayouza filamu kutoka nje bila kulipa kodi.

Ukiongelea suala la ulipaji kodi unawagusa mamlaka ya Mapato (TRA) kwanini filamu za ndani zibanwa kulipa kodi na za nje zinazokuja kwa njia ya wizi (Piracy) ziuzwe kwa bei rahisi tena bila kulipia ushuru, ni changamoto tuone mwaka mpya na awamu mpya.

Aidha lawama inayowahusu wasambazaji moja kwa moja ni kuhusu ubunifu kupungua katika utunzi wa filamu zetu kwani inasemekana kila siku sinema zina hadithi za aina moja tu, huku washiriki nao wakibadirisha mavazi tu, lakini kila kitu kikijirudia na watazamaji kuona hakuna jipya.

Uzushi kwa mwaka 2015
Kama ilivyokuwa waswahili usema mazoea ujenga tabia hivi sasa watu maarufu sambamba na wasanii wetu wasanii wetu wamekuwa wepesi sana kuposti maneno ya hisia kwa wafiwa wakiwapa pole bila hata uhakika, mtu mmoja anasema kuwa si rahisi watu kumjulia hali lakini ni mabingwa wa Rest In Peace.

Mwaka jana habari za kusitusha ziliripotiwa kutoka Bagamoyo zikidai kuwa msanii nyota na mkongwe katika uigizaji Thecla Mjatta ‘Mama Mjatta kuwa amefariki na watu kumiminika na R.I.P Mama Mjatha kumbe habari hizi zilikuwa ni uzushi na kuiacha familia ya mama huyo katika sintofahamu na usumbufu.
TAFF
Pamoja na mikasa au soko kushuka lakini kuna watu ambao walipigania na tasnia na kuweka njia na mwelekeo ambao ni shirikisho la Filamu Tanzania (TAFF) pamoja na kupigania urasimishaji wa filamu kwa kushirikiana na wadau waliweza kufanikisha utoaji wa Tuzo za TAFA zilizofana.

Pia mwaka huu ulikuwa wenye faida kwa mtayarishaji na muongozaji wa filamu Timoth Conrad ‘Tico’ baada ya kuibuka kidedea kwa kupata tuzo nyingi kutoka Marekani na kuipaisha Tanzania katika anga za filamu ughaibuni.

Katika taasisi ambayo inastahili sifa ni Bodi ya Ukaguzi wa Filamu na Michezo ya kuigiza chini ya Katibu Mtendaji Mama Fisso kutoa elimu kwa watengenezaji wa filamu na kuweza kupeleka filamu zao kukaguliwa kuingia mtaa tofauti na siku za nyuma ambapo hawakuona umuhimu wa kukagua filamu.

Ni baadhi ya matukio machache yaliyopita kwa mwaka uliopita na sasa mwaka mpya umeingia kukiwa na changamoto nyingi ambazo zinatakiwa kufanyiwa kazi ili kurudisha soko katika ubora wa awali na kila mtu awajibike kwa sehemu yake.

RIPOTI NA FILAMUCENTRAL

Comments

comments

Exit mobile version